WIKI iliyopita nilizungumzia juu ya Tanzania
tunayoitaka, ambapo kimsingi nilieleza sifa za viongozi ambao tunatakiwa kuwa nao
katika taifa letu.
Pamoja na mambo mengi niliyoyaeleza katika
makala hayo, pia nilisema tunahitaji kuwa na taifa lenye viongozi wanaowajibika,
wenye kutenda haki, kujali haki za binadamu, kutumika kwa maslahi ya umma, wenye
kukataa rushwa ndogo na kubwa, watakaotuongoza katika mafanikio ya kweli na
watakaokataa kutumika kwa maslahi ya vyama vyao bali kwa maslahi ya Watanzania
wote.
Leo katika safu hii nimeona ni vyema
nikazungumzia kuhusu rushwa ambayo imekuwa ikihusisha wanasiasa na wananchi
hasa katika kipindi cha uchaguzi.
Tutakumbuka kwamba katika miaka ya karibuni
wawakilishi wetu walifikia hatua ya kubariki rushwa ambayo ilibatizwa jina la ghiliba
la ‘takrima’.
Takrima ilikuwa ni kutoa ruksa kwa mwanasiasa
anayegombea nafasi fulani ya madaraka hapa nchini; iwe urais, ubunge au udiwani
kumpatia kitu kidogo mpiga kura kama njia ya kumshukuru.
Takrima hiyo ikaruhusu mtu kumshukuru mpiga kura
wake hata kabla ya uchaguzi. Ilikuwa ruksa kumpatia pesa, nguo, chakula na
zawadi nyingine yeyote mtu ambaye unadhani angeweza kukupigia kura.
Hata hivyo, takrima haikudumu kwa kipindi
kirefu, wale wale waliofikiria na kuibariki walifikia uamuzi wa kuiondoa na
kusema kuwa ni rushwa. Neno takrima likaishia hapo kutumika, lilikosa mvuto, lilitelekezwa
na hakuna aliyelitumia tena.
Hali halisi ya mazingira ya kisiasa hapa nchini
inaonyesha kuwa neno takrima lilikufa, lakini kivuli chake bado kinaishi.
Wengi mtakubaliana nami kuwa, fedha, sabuni, fulana,
kofia, khanga bado zinatolewa bure kwa wananchi, iwe kipindi cha karibu na
uchaguzi au katika uchaguzi wenyewe.
Hizi ni zawadi zinazotolewa na baadhi ya
wagombea katika nafasi mbalimbali za uongozi hapa nchini kwa wananchi, ili tu
wachaguliwe kushika nafasi za madaraka.
Wananchi wanaoishi kwenye lindi la umaskini, ambao watoto wao wanasoma kwenye vyumba vya madarasa vilivyoezekwa kwa nyasi, huku wabunge na madiwani wakitafuna posho za vikao bila hata mshipa wa aibu kuwashtua, wamekuwa wakidanganywa kwa khanga na fulana hadi kuamua kuwapa tena nafasi ya uwakilishi waheshimiwa hao hao.
Wananchi wanaoishi kwenye lindi la umaskini, ambao watoto wao wanasoma kwenye vyumba vya madarasa vilivyoezekwa kwa nyasi, huku wabunge na madiwani wakitafuna posho za vikao bila hata mshipa wa aibu kuwashtua, wamekuwa wakidanganywa kwa khanga na fulana hadi kuamua kuwapa tena nafasi ya uwakilishi waheshimiwa hao hao.
Mbunge au diwani kuamua kutoa zawadi za namna hiyo kwa wapiga kura wake ili
wamchague tena ni ishara ya kuwa hakufanya kazi yake ipasavyo kipindi
kilichopita.
Pamoja na majukumu mengine aliyonayo mbunge,
anapaswa kuisimamia serikali ili iweze kuwajibika ipasavyo kwa wananchi ambao
ndio wenye nchi. Madiwani pia wana jukumu hilo.
Hawa ni wawakilishi wetu, ndio wanaowakilisha Watanzania
wote katika kuidai serikali haki zetu. Iwe huduma nzuri za kijamii, mfano;
shule, hospitali na nyingine.
Kwa nini waidai serikali na wasifanye wao? Kimsingi
katika utawala huu wa kidemokrasia, serikali na wananchi wapo katika uhusiano (relationship).
Kwa sababu ya uhusiano uliopo baina ya wananchi
na serikali; serikali ikiwa mbeba majukumu na wananchi wakiwa ‘wenye haki’
(rights holders) ni lazima serikali iwajibike kwa wananchi.
Hivyo, serikali ndiyo baba na mama wa wananchi
na mbunge na diwani ndio kaka mkubwa wa wananchi. Mbunge na diwani wanatakiwa
kuwa katika sura ya mwananchi wa kawaida na kazi yao kubwa ni kumwambia baba na
mama kuwa sisi huku tunataka shule, hospitali, barabara ni vitu vingine vingi. Siyo
wao kuanza kutoa fedha zao na kufadhili wananchi kwa vitu vidogo vidogo ili
wawaone ni watu wema.
Kutoa fulana, khanga, fedha na zawadi nyingine
kwa wananchi ni kutoa rushwa. Rushwa
iliyogeuzwa kuwa uwajibikaji kwa wananchi na wao wakakubali na kushangilia kuwa
mbunge au diwani anatujali.
Hiki
ni kivuli cha takrima na jamii inapaswa kutambua kuwa hii ni rushwa na wala siyo
uwajibikaji.

No comments:
Post a Comment