Wednesday, July 11, 2012

Shule zinakosa Chaki, tunawaongeza madiwani posho

“WAKATI nahitimisha mjadala wa hotuba ya bajeti ya ofisi yangu mwaka jana, niliahidi kuwa Serikali itaangalia upya viwango vya posho za madiwani kwa lengo la kuviongeza,” alisema Pinda na kuongeza;


“Sasa zoezi hilo limekamilika na kuanzia mwaka 2012/2013 madiwani watalipwa viwango vipya vya posho vilivyoboreshwa.” Gazeti la Mwananchi la Jumatatu , tarehe 25 Juni mwaka huu, lilimkariri    Waziri Mkuu, Mizengo Pinda akitamka maneno hayo, wakati akisoma hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu (Tamisemi), kwa mwaka 2012/13.

 

Pinda ametangaza kuongeza posho za madiwani akijitetea kuwa anatimiza ahadi yake ya mwaka uliopita wa fedha.Kufanya hivyo kwa Pinda ni kuwafurahisha na kuwaridhisha madiwani hivyo kufanya waipende serikali na kuiabudu.

 

Wafanyakazi wengi wa serikali  wamekuwa wakilalamika juu ya mishahara midogo, posho ndogo au hakuna kabisa; lakini hawapati wanacho lalamikia kwa serikali.

 

Maisha ya Mtanzania wa kawaida yamekuwa magumu kwa sasa, kiasi kwamba hata familia zipo hatarini kusambaratika.Baba hana kitu na mama hana kitu,watoto wanapiga miayo muda wote.

 

Kwenye vituo vya afya, zahanati na hospitalini karibu kote nchini mara kwa mara wauguzi/madaktari wanawajibu wagonjwa  kuwa hakuna dawa.Wakanunue madukani.

 

Kwenye shule za msingi za umma , ‘kaumba’, hakuna vitabu,chaki na madawati ya kutosha. Wanafunzi wanakaa wanne mpaka watano katika dawati moja.

 

Walimu wanatoa fedha zao mifukoni kununua chaki, na wazazi wanaelezwa kuwanunulia watoto wao vitabu kwani hali ni mbaya.

 

Fedha za rudhuku kwa maendeleo ya shule ni kitendawili.Katika baadhi ya shule nchini hazifiki kabisa, kwingine zinachelewa kufika na zikifika zinakuwa kidogo.

 

Mfano,ofisa mtendaji katika kata moja huko wilayani Mufindi alinieleza kuwa katika kata yake, fedha ya rudhuku iliyoletwa katika baadhi ya shule ni shilingi 20,000 tu, haitoshi hata nauli ya mtu anaetoka kijijini huko kwenda mjini mafinga kununua vitendea kazi vya shule.

 

Hali hii ya maisha magumu katika jamii, ambayo ni ashirio la kudorora kwa  uchumi wa nchi, inawaumiza sana wananchi maskini hasa ukizingatia hata huduma za kijamii zinazopaswa kutolewa bure au kwa unafuu kama huduma za afya na elimu nazo hazitolewi kwa kuridhisha.

 

Wakati Pinda anatangaza kuongeza posho za madiwani, wabunge walishangilia kwa kishindo.Nini maana yake?Mimi na wewe tujiulize.

 

Kadri siku zinavyosonga mbele hali ya uendeshwaji wa shule zetu za misingi za umma inazidi kuwa mbaya.Walimu wamekosa matumaini ya kuishi na kufanya kazi kwa moyo mmoja.

 

Wengi wamechakaa,wamepauka na kuonekana wazee wakati bado vijana .Serikali ipo kimya,wanafunzi wanakosa vifaa muhimu, wanatimiza wajibu tu wa kuwa shule, na kusogeza siku mbele.

 

Tumefikia kipindi shule zetu zinaendeshwa kwa fedha za michango ya wananchi, walizochanga kwa ajili ya maendeleo mengine ya vijiji vyao.

 

Wenyeviti wa vijiji wameamua kutumia michango iliyochangwa kwa ajili ya kazi nyingine ili kusaidia wanafunzi waendelee kupata elimu lakini bado tunawalaumu kwa kufanya hivyo.

 

Mfano,mwezi uliopita iliripotiwa katika vyombo vya habari kuwa, ‘Mkuu wa Wilaya ya Kilolo mkoani Iringa, Gerald Guninita amemkamata na kumweka chini ya ulinzi, Mwenyekiti wa Serikali ya Kijiji cha Udekwa kilichopo Tarafa ya Mahenge, Obadiah Lubugo, kwa kutochangia Sh.70,000 za Mbio za Mwenge’. 

 

‘Lubugo, ambaye ni Mwenyekiti wa Serikali ya Kijiji kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), alionja kadhia hiyo
baada ya kuelekeza fedha hizo katika manunuzi ya chaki
kwenye Shule ya Msingi Udekwa’.Mwisho wa kunukuu.

 

Lubugo amejitetea kuwa alifanya hivyo baada ya kuona shule haina chaki na wanafunzi hawasomi kutokana na kukosekana kwa chaki, lakini ameonekana kapotoka na kukosea.

 

Lakini kulingana na hali halisi ilivyo sasa katika shule hizo za umma, alichofanya mwenyekiti huyu, kutoa fedha za kijiji zilizokusudiwa kutumika kwa kazi nyingine ili kununulia chaki na kufanikisha wanafunzi kufundishwa, kimekuwa kikifanywa  na wenyeviti wengine wa vijiji mara kwa mara.

 

Tunakwenda wapi? Shule zinakosa chaki, sisi tunawaongeza madiwani posho.

CHANZO: KWANZA JAMII-IRINGA


No comments:

Post a Comment