Saturday, July 7, 2012

Ngoma ya Sungura yaweza kuleta mabadiliko chanya

HAPO zamani za kale, kulikuwa na shida kubwa sana ya maji katika nchi zote. Kwa bahati, likabakia ziwa moja tu. Wanyama wengi wa kila aina walipata maji yao kwenye ziwa hilo. Wanyama wakubwa kama vile Tembo, Simba na Chui; waliwanyanyasa sana wanyama wadogo waliofika kunywa maji kwenye ziwa hilo. Wakawa hawana raha. Walipata maji kwa shida sana baada ya manyanyaso makali.

Sungura alipoona hivyo, alianza kukuna kichwa akifikiri jinsi ya kuepukana na adha hiyo. Akapata njia. Alitengeneza ngoma na kucheza kwa siri nyumbani kwake. Wanyama wengine waliposikia sauti ya ngoma ile ilivyosikika vizuri, wakavutiwa nayo. Wa kwanza kuvutiwa, walikuwa wanyama wakubwa. Wakamwendea Sungura ili wapate kuiona ile ngoma inayotoa sauti nzuri. Sungura akawaambia: “Mimi napiga ngoma hiyo na kucheza peke yangu kwa siri. Ninyi mkitaka kuiona, naomba mje mmoja mmoja, nami nitawaonyesha.” Hiyo ilikuwa mbinu yake tu kutaka kujua nani atakuwa wa kwanza na wa mwisho kuja kwake ili apate kuwatenda vibaya.

Tembo alikuwa wa kwanza kwenda kwa Sungura. Akamwambia: “Ingia nyumbani mwangu”. Tambo bila kukawia akaingia ndani. Loo, maskini Tembo! Sungura akafunga mango kwa Nguvu, mara akachoma nyumba yote. Tembo akafa.

Akaja Chui, bila kufahamu kilichotekea kwa Tembo. Yeye akapelekwa kwenye mlima wa mawe wenye mtelemko mkali. Sungura akamwambia: “Hapa wanapatikana wanyama wengi sana. Unisaidie kuwinda ili upate kula karamu kabla ya kucheza ngoma. Wanyama wanapatikana kwa urahisi sana ukifuata taratibu nitakayokuelekeza. Nayo ni hii: Ufumbe macho mpaka mnyama anapoanza kukupita. Kisha, ufumbue macho na umfuate kwa nyuma. Ndipo utakapofaulu kumkamata”.

Chui akakubali. Sungura akapanda mlimani kuporomosha jiwe kubwa. Likaja moja kwa moja kutoka juu na kumponda Chui aliyefumba macho kungoja mnyama. Sungura akamchukua Chui na kumchuna ngozi. Zamu ya Simba ilifika, akamwmbia: “Ngoma hii kila atazamaye, lazima achunwe ngozi kama walivyofanya wenzako. Tazama, ngozi hii ni ya nani? Si ya Chui?” Simba akakubali. Akachunwa kwa tamaa ya kutazama ngoma, akafa. Sungura Akava ngozi hizo kwa zamu ili kwenda ziwani kuwatishia wanyama wadogo. Sungura akatawala maji yale, wakati Wote wa shida, kutokana na werevu wake.
Hadithi hii tamu yenye mafunzo mengi, nilipata  kuiona katika wavuti na ilielezwa kuwa imetungwa na  Kat.V:A Ndunguru.
Kwa mtazamo wangu,sungura hapa ni shujaa,alitumia akili yake kuweza kupata maji ambayo yalikuwa bidhaa adhimu kwa wanyama wengi wadogo.
Hebu tuangalie,maisha yetu watanzania wakawaida na ya baadhi ya viongozi wetu tuliowachagua wenyewe kutuongoza.
Wengine wanaishi kama miungu watu,hawaguswi,hawasogelewi,wanatunyanyasa na sisi tunalalamika tu.Hatuchukui hatua.
Tunafahamu fika habari za baadhi ya wabunge wetu kuwa na viburi kwa wapiga kura kiasi cha kufikia kusema kwenye kampeni “Mnichague msinichague mimi ni mbunge wenu tu”
Haya ni manyanyaso kama ambayo walifanyiwa sungura na wanyama wenzake wadogo.
Tofauti yetu na sungura ni,sisi si wajanja kama yeye.Sisi ni wapole ,lakini si wakimya kwa sababu ni mabingwa wa kulalamika.
Hakuna lolote la maendeleo tulilofanyiwa na mbunge au diwani wetu kwa kipindi chote cha uongozi wake,lakini akija na kipande cha sabuni tu wakati wa uchaguzi;tunamkubali,tunamchagua tena tunaendelea kulalamika.Basi mchezo wetu ni huo.
Ninafikiri tujifunze kwa sungura kwani,hakuwa tayari kupewa bakuli au ndoo ya maji kwa siku moja ili awaone akina simba,tembo na wanyama wengine wakubwa ni watu wema.
Tutumia ngoma,tuwaalike ngomani,waje,tumalize jeuri zao wale wote wanaotufanya tuteseke.Tuwapigie kura ya siyo,ambayo maumivu yake kwao itakuwa kama kifo.

Ngoma yetu ni uchaguzi,uchaguzi mkuu wa mwaka 2015 , tunauelekea sasa.Tufanye kweli.

No comments:

Post a Comment